Abstract apocalyptic background - burning and exploding planet Earth in red sky, hell, end of world. Elements of this image furnished by NASA

Namna Nabii Isa (‘alaihis salaam) alivyozaliwa

Mfumo wa Allah Ta‘ala, kuhusiana na jinsi mwanadamu alivyo umbwa, ni kwamba wakati mambo mawili yanapopatikana basi mwanadamu atapatikana. Sababu ya kwanza ni njia ya wazazi ambayo mbegu ya mwanaume hupandwa ndani ya tumbo la mama. Sababu ya pili ni roho kupulizwa ndani ya tumbo baada ya kukamilisha miezi minne.

Kila mtu aliyekuja duniani alifuata mfumo huu. Lakini, Allah Ta’ala amewafanya watu watatu kuwa tofauti na kanuni hii yaani Nabii Aadam, Hawwaa, na Nabii Isa (‘alaihimus salaam).

Kuhusiana na Nabii Aadam (‘alayhis salaam), Allah Ta’ala aliutengeneza umbo lake na mchanga na kisha akapuliza rooh ndani yake. Kwa hivyo, alizaliwa bila njia ya wazazi wawili.

Ama Hawwaa (‘Alaihas salaam), Allah Ta‘ala alimuumba kutoka ubavu wa kushoto wa Nabi Aadam (‘alayhis salaam). Kwa hivyo, alizaliwa kupitia njia ya mwanamume tu.

Ama Nabii Isa (‘alaihis salaam), basi Allah Ta’ala alimuumba kwa kupuliza roho ndani ya tumbo la mama yake. Kwa hiyo, alizaliwa kupitia njia ya mwanamke pekee.

Katika Qur-aan Majeed, Nabii Isa (‘alayhis salaam) amefananishwa na Aadam (‘alayhis salaam). Allah Ta’ala Anasema:

Hakika mfano wa Nabii Isa (‘alayhis salaam) kwa Mwenyezi Mungu ni sawa na mfano wa Nabii Aadam (‘alayhis salaam). Allah Ta’ala alimuumba (Nabii Aadam) na mchanga, kisha akauambia (mchanga): “Kuwa! naye akatokea.” (Sura Aal–Imraan aya ya 59)

Katika Aaya hii, Allah Ta‘ala anaeleza kwamba uumbaji wa Nabii Isa (‘alaihis salaam) ulifanana na uumbaji wa Nabii Aadam (‘alaihis salaam) kwa maana ya kwamba Nabii Aadam (‘alayhis salaam) hakuzaliwa kupitia njia ya wazazi, bali aliumbwa na ruhu kupulizwa ndani yake.

Vile vile, Nabii Isa (‘alayhis salaam) hakuzaliwa kupitia njia ya baba, kwa sababu Ruhu ulipulizwa tumboni mwa mama yake, na kusababisha yeye kuwepo.

Kwa hivyo, tunaona kwamba kama jinsi uumbaji wa Nabi Aadam (‘alayhis salaam) na Hawwaa (‘alaihas salaam) ulivyotokea na mujiza, hivyo hivyo uumbaji wa Nabii Isa (‘alayhis salaam) ulikuwa wa kimujiza.

Miujiza wa Nabii Isa (alayhis salaam)

Allah Ta’ala alimbariki Nabii Isa (‘alayhis salaam) kwa uwezo wa kufanya miujiza nyingi. Kila muujiza alioufanya ulifanywa kwa idhini ya Allah Ta’ala, na kupitia kwa Allah Ta’ala akimwezesha na kumpa uwezo wa kuitekeleza.

Miongoni mwa miujiza aliyoifanya, kama ilivyotajwa katika Qur-aan Majeed, ni kwamba atawaponya wenye tatizo na ngozi na waliozaliwa vipofu. Alitengeneza viumbe vya ndege kwa udongo na kisha akapuliza kwenye umbo hili, na Allah Ta’ala akazihuisha.

Allah Ta’ala Akimnyanyua Nabii Isa (‘alayhis salaam) Mbinguni

Kuhusu Nabii Isa (‘alaihis salaam), Wakristo wanaamini kwamba alisulubishwa msalabani na aliuawa na Mayahudi. Lakini, imani hii ni ya uwongo na imekataliwa waziwazi ndani ya Qur-aan Majeed.

Imani ya Uislamu ni kwamba Mayahudi hawakufaulu kumuua, lakini Allah Ta’ala alimuokoa na madhara yao na akampandisha mbinguni kwa muujiza. Allah Ta’ala anafafanua hili kwa uwazi kabisa katika Qur-aan Majeed. Allah Ta’ala Anasema, “Na hawakumuua (Mayahudi) wala hawakumsulubu, bali jambo hilo liliwavuruga.  Hakika wale waliobishana katika jambo hili wamo katika shaka nalo.  Hawana ujuzi nalo, lakini wanafuata dhana. Ni hakika kabisa kwamba hawakumuua, lakini Mwenyezi Mungu alimnyanyua kuelekea Kwake. Mwenyezi Mungu ni Mwenye nguvu, Mwenye hikima.” (Sura Nisaa aya 157-158)

Kutokana na hayo hapo juu, tumeona kwamba maisha ya Nabii Isa (‘alayhis sallam) ni kielelezo cha wazi cha Qudra (nguvu) wa Mwenyezi Mungu (subhaanahu wata’ala). Kutokana na namna ya pekee aliyozaliwa na miujiza aliyoifanya hadi namna ya kimiujiza ambayo Allah Ta‘ala alimpandisha mbinguni – vyote vinadhihirisha uwezo wa Allah Ta’ala.

Dajjaal atakapokuja duniani, atakuwa akifanya fitna kubwa na uharibifu ulioenea duniani. Fitnah yake, kama ilivyotajwa katika Hadith, itakuwa ni fitna kubwa kabisa ambayo dunia haijawahi kuishuhudia tangu mwanzo wa dunia. Katika wakati huo muhimu, itakuwa ni Nabii huyu mkubwa wa Allah Ta‘ala – Nabii Isa (‘alayhis salaam), ambaye ni dhihirisho la Qudra wa Allah Ta’ala, ambaye atatumwa duniani na Mwenyezi Mungu kuuokoa umma wa Mtume (Sallallahu alaihi wasallam) kwa kumuua Dajjaal, na kuimaliza fitna yake.

About admin

Check Also

Mahdi (Radhiya Allaahu ‘anhu)

Kuja kwa Mahdi (Radhiya Allaahu ‘anhu) ni dalili ya kwanza kati ya alama kuu zitakazojitokeza …