وَالنَّازِعَاتِ غَرْقًا ﴿١﴾ وَالنَّاشِطَاتِ نَشْطًا ﴿٢﴾ وَالسَّابِحَاتِ سَبْحًا ﴿٣﴾ فَالسَّابِقَاتِ سَبْقًا ﴿٤﴾ فَالْمُدَبِّرَاتِ أَمْرًا ﴿٥﴾
Ninaapa kwa wale (malaika) ambao wanao toa (roho za makafiri) kwa nguvu, na kwa wale (malaika) wanao toa (roho za waumini) kwa upole, na kwa wale (malaika) ambao wanapaa (angani) kwa haraka, na kwa wale (malaika) ambao wanashindana mbio (kutimiza amri za Allah Ta’ala), na wale (malaika) ambao wanasimamia mambo (wameamriwa kutimiza na Mwenyezi Mungu subhaanahu wata’ala,)
Kama vile Surah iliopita – Surah Naba – iliteremshwa kuthibiti imani ya siku ya Qiyamaah, hivyo Surah hii pia iliteremshwa kujadili mambo kadhaa ya Qiyaamah.
Katika Surah hii, Mwenyezi Mungu (subhaanahu wata’ala) anaanza na kuchukua viapo juu ya sifa fulani za malaika ili kudhibitisha kwamba siku ya Qiyaamah ni hakika. Kwa hivyo, katika aya ya sita, baada ya kuchukua kiapo juu ya sifa za malaika, Mwenyezi Mungu (subhaanahu wata’ala) anasema juu ya siku ya Qiyaamah.
Sababu dhahiri ya Mwenyezi Mungu (subhaanahu wata’ala) kuchukua viapo kwa malaika ambao huondoa roho za watu ni kumjulisha mwanadamu kwamba kila mtu qiyaamah yake itaanza baada ya kufariki. Kwa hivyo, inasemekana, “Yule anayefariki, Qiyaamah yake inaanza.”
Ingawa Qiyaamah halisi kwa viumbe wote itafanyika mwishoni mwa ulimwengu, hata hivyo kwa kuwa maisha ya aakhera ya kila mtu itaanza wakati wa kifo chake, kifo cha kila mtu kinahesabiwa kuwa Qiyaamah yake.
Kwa jumla, katika aya hizi, Mwenyezi Mungu (subhaanahu wata’ala) anaangazia sifa tano za malaika. Sifa tano ni hizi zifuatavyo:
Sifa ya kwanza ya malaika
وَالنَّازِعَاتِ غَرْقًا ﴿١﴾
Ninaapa kwa wale (malaika) ambao hutoa (roho za makafiri) kwa nguvu
Katika aya hii, Mwenyezi Mungu (subhaanahu wata’ala) anaongea juu ya malaika wa kifo ambao hutoa roho za makafiri kwa nguvu na kwa ukali, kwa nguvu kamili, bila kuwaonyesha huruma yoyote. Malaika ambao huondoa roho za makafiri ni malaika wa adhabu, na neno “kwa nguvu” katika aayah linamaanisha maumivu ya kiroho, sio maumivu ya mwili. Kwa hivyo, watu ambao wapo karibu na mtu anayekufa hawawezi kuona maumivu ya mtu anayekufa kwa sababu maumivu yanahisi na roho ya mtu anayekufa, na sio mwili wake.
Wakati mwingine, inaonekana ingawa roho ya kafiri inatoka kwenye mwili wake kwa urahisi, lakini kwa ukweli sio hivyo, kama ilivyo katika aya hii, Allah Ta’ala anatuarifu juu ya uchungu mkubwa na mateso ambayo roho ya kafiri hupitia wakati wa kifo.
Sifa Ya Pili Ya Wa Malaika
وَالنَّاشِطَاتِ نَشْطًا ﴿٢﴾
na kwa wale (malaika) wanao toa (roho za waumini) kwa upole
Katika aya hii, Allah Ta’ala anasema kuhusu wamalaika ambao hutoa roho za waumini vizuri na kwa upole. Malaika ambao huondoa roho za waumini ni malaika wa huruma. Wameamriwa na Mwenyezi Mungu (subhaanahu wata’ala) kushughulika na waumini kwa njia ya fadhili na upole.
Neno “النَّاشِطَاتِ“ limetoka kwenye neno “نشطَ” ambalo linamaanisha “kufungua fundo”. Hii inaashiria “kuondoa fundo la kitu ambacho kina maji au hewa, ili maji au hewa iweze kutolewa kwa urahisi”. Hii ni mfano wa kutoa roho za waumini kwa upole, tofauti na roho za makafiri ambao hutolewa kwa ukali. Ni kama roho ya muamini ilikuwa imefungwa ndani ya mwili wake, na mwili ulihitaji kufunguliwa kwa roho kutolewa.
Katika kesi hii pia, neno نَشْطًا ambalo hutafsiri kama “vizuri” au “kwa upole” linamaanisha kwa ulaini au upole, na sio uzoefu wa mwili. Wakati mwingine, mwamini mcha Mungu huonekana akipitia ugumu wa aina fulani wakati wa kifo chake, lakini hii haimaanishi kuwa anapitia ugumu wa kiroho au adhabu, ingawa kimwili inaweza kuonekana kwa wale waliopo karibu naye.
Wakati roho ya makafiri inapotolewa, eneo lote la adhabu ya Barzakh (maisha baada ya kifo) linakuja mbele yake. Ni wakati wa hofu kubwa na ya kutisha, na mtu anayekufa amezidiwa na hali hiyo. Kwa hivyo roho ikiwa na hofu sana na adhabu, huanza kutoka kwenye mwili wote, kujaribu kujificha au kutoroka adhabu. Lakini Malaika wa Kifo huondoa roho yake kwa nguvu na kwa ukali kutoka mwili wake, kama vile chuma hutolewa kwa nguvu kwenye uzi la kurowa (kama ilivyoelezewa katika Hadith ya Baraa bin Aazib (Radhiyallahu ‘Anhu) iliyorekodiwa katika Musnad-Ahmad).
Kwa upande mwingine, wakati roho ya mwamini inapotolewa, thawabu kubwa na baraka za Akhera ambazo ziko karibu kwake zinawasilishwa mbele yake na anapewa habari njema, kwa hivyo, roho yake inaacha mwili wake kwa urahisi na furaha.
Sifa Ya Tatu Wa Malaika
وَالسَّابِحَاتِ سَبْحًا ﴿٣﴾
na kwa wale (malaika) ambao wanapaa (mbinguni) kwa haraka
Katika aaya hii, Mwenyezi Mungu (subhaanahu wata’ala) anaeleza sifa ya tatu ya wamalaika. Malaika waliotajwa katika aya hii ni malaika wa kutoa roho ambao, baada ya kutoa roho ya mwanadamu, hutembea haraka mbinguni wakichukua roho kuelekea angani ili kuiwasilisha mbele ya Mwenyezi Mungu (subhaanahu wata’ala).
Neno “سٰبحٰت” linatoka katika neno “سبح” ambalo linamaanisha “kuogelea” au “kuelea”, lakini katika muktadha huu, kuhusiana na malaika, maana ya hilo neno ni “kupaa mbinguni haraka”.
Sifa Ya Nne Ya Wamalaika
فَالسَّابِقَاتِ سَبْقًا ﴿٤﴾
na kwa wale (malaika) ambao wanashindana mbio (kutimiza amri za Allah Ta’ala),
Katika aaya hii, Mwenyezi Mungu (subhaanahu wata’ala) anaongea juu ya jinsi malaika wa kutoa roho wanashindana na kila mmoja kutimiza amri ya Mwenyezi Mungu (subhaanahu wata’ala).
Kulingana na Amri ya Mwenyezi Mungu (subhaanahu wata’ala), malaika huchukua roho za wachamungu kwa makao yao mazuri, na roho za waovu kwa makao yao mbaya. Baada ya kuhojiwa kaburini, roho ya waumini husafirishwa kwenda makao ya Illiyyeen ambapo itafurahishwa na baraka za pepo, na roho ya makafiri zinasafirishwa kwenda Sijjeen ambapo itateseka kwa kuteswa motoni. (Al-Rooh pg. 134)
Sifa Ya Tano Ya Wamalaika
فَالْمُدَبِّرَاتِ أَمْرًا ﴿٥﴾
na wale (malaika) ambao wanasimamia mambo (wameamriwa kutimiza na Mwenyezi Mungu subhaanahu wata’ala,)
Katika Aaya hii, Mwenyezi Mungu (subhaanahu wata’ala) anasema kuhusu hao malaika ambao husimamia maswala ya marehemu na kutimiza kile wanachoamrishwa na Mwenyezi Mungu (subhaanahu wata’ala) katika kuwapa thawabu roho za wacha Mungu na kuwaadhibu roho za waovu.
Kwa maneno mengine, kazi ya mwisho ya malaika hawa wa kifo itakuwa kuleta faraja kwa zile roho za wachamungu na kusababisha maumivu kwa roho za waovu. Baada ya roho kufikia makazi yao mema au mabaya, malaika ambao wameamrishwa kuwalipa na kufariji roho za wachmungu hukusanya vitu vya thawabu na faraja kwa ajili yao, na malaika ambao wameamrishwa kuadhibu na kusababisha maumivu kwa roho za waovu hupanga njia kwa adhabu na maumivu yao.
Thawabu na adhabu katika kaburi
Surah hii hadi sasa inathibitisha kwamba wakati wa kifo, malaika watafika na kutoa roho ya mwanadamu. Halafu wataipeleka angani na kusafirisha kupeleka makao yao. Nafsi nzuri itasafirishwa kwenda kwenye makao mazuri, na roho za waovu itasafirishwa kwenda kwenye makazi mabaya. Huko malaika watapanga njia za malipo na faraja, au adhabu na maumivu kwa aina zote mbili za roho.
Aya zinaonyesha kuwa malipo na adhabu itafanyika kaburini (i.e. katika maisha ya Barzakh baada ya mtu kuondoka ulimwenguni). Baada ya hapo, siku ya Qiyaamah itakapokuja, uamuzi utapitishwa kwa mtu gani atapewa Jannah, na ni mtu gani atakayepangwa kwenda motoni.
Kuhusu jinsi roho ya mcha Mungu au mwovu hutolewa na malaika wa kifo, kuna hadithi ndefu ya Baraa bin Aazib (Radhiyallahu ‘Anhu) iliyoripotiwa katika Musnad Ahmad. Hadith ni kama ifuatavyo. Baraa bin Aazib (Radhiyallahu ‘Anhu) anaripoti:
Katika hafla moja, tulitoka na Rasulullah (Sallallahu ‘Alaihi Wasallam) kuhudhuria Janaazah ya mtu wa Ansaar. Tulipofika kaburini, tuligundua kuwa kaburi lilikuwa bado halijachimbwa. Rasulullah (Sallallahu ‘Alaihi Wasallam) kwa hivyo alikaa chini, na tukakaa karibu naye kwa utulivu hadi kulikuwa na ndege juu ya vichwa vyetu.
Rasulullah (Sallallahu ‘Alaihi Wasallam) alikuwa na fimbo mikononi mwake ambayo alikuwa akipiga ardhi (kwa kufikiria sana). Rasulullah (Sallallahu ‘Alaihi Wasallam) kisha akainua kichwa chake na kusema mara mbili au mara tatu, “Jikingeni kwa Allah Ta’ala na adhabu ya kaburi!”
Baada ya hapo, Rasulullah (Sallallahu ‘Alaihi Wasallam) alisema, “Kwa kweli, wakati mwamini anakaribia kuondoka katika ulimwengu huu na kwenda Akhera, basi Malaika hushuka kwake kutoka mbinguni. Uso wao mweupe sana na kung’aa kama jua. Watakuwa nao pamoja nao ni sanda la hariri sanda la Jannah, na manukato kutoka Jannah. Watakaa karibu naye sehemu ataweza kuwaona.
“Baada ya hapo, malaika wa kifo atakuja kwake na kukaa kando ya kichwa chake. Malaika wa kifo atamwambia akisema, ‘Ewe roho safi! Toka, kuelekea msamaha wa Mwenyezi Mungu na furaha yake!’ Kwa hivyo roho itatoka (vizuri), kama jinsi tone la maji linatoka kwenye maji.
“Malaika wa kifo basi hushikilia roho, na mara tu atakaposhikilia, malaika wengine pamoja naye hawaachi mikononi mwao hata sekunde moja hadi watakapoichukua na kuiweka ndani ya kitambaa na manukato (manukato ya Jannah). Harufu hutolewa kutoka kwenye roho ambayo ni harufu nzuri zaidi kuliko manukato mazuri ya musk yanayopatikana duniani.
“Malaika basi hupanda angani na roho, na kikundi chochote cha malaika wanaopita, malaika hao wanauliza kutoka kwao, ‘ni roho la nani ilio safi hivi?. Malaika watajibu ni fulani bin fulani, wakimtaja na majina mazuri ambayo walikuwa wakimwita nazo duniani.
“Malaika wanaendelea kupaa na roho hadi watakapofika mbingu la kwanza. Wakifika mbingu la kwanza, wanaomba rukhsa ya kuingia. Mlango wa Mbingu utafunguliwa kwa ajili yao, baada ya hapo malaika wa mbingu hiyo watakaribisha roho na kuipeleka katika mbingu nyingine, na hili litaendelea kwa kukupitia kila mbingu, mpaka roho itakapofika mbingu ya saba.
“Mwenyezi Mungu (subhaanahu wata’ala) kisha anawamuru malaika wakisema, ‘Andika katika kitabu cha mja wangu kwamba makao yake yameamuliwa kuwa ndani ya Illiyyeen, na kisha kumrudisha duniani (yaani. Mchukue kwenye kaburi lake kwa kuhojiwa), kama nilivyowaumba kutoka kwenye ardhi, nitawarudisha kwenye ardhi, na nitawafufua tena kutoka kwenye ardhi. ‘
“Nafsi inarudishwa kwenye mwili ndani ya kaburi ambalo malaika wawili ( Munkar na Nakeer) huja kwake. Watamkalisha na kumuuliza, ‘Mola wako ni nani?’ Atajibu, ‘Mola wangu ni Allah. Kisha watamuliza dini yako ni dini gani? Atajibu, ‘dini yangu ni Islam. Mwishoni watamuliza huyu ni nani ambaye alitumwa kwako? Atajibu, ‘Yeye ni Rasulullah (Sallallahu ‘Alaihi Wasallam).’ Malaika watauliza, ‘Je! Unajuaje hii? Atasema, ‘nasoma kitabu cha Allah Ta’ala na nimeleta imani kwake na nimekubali kuwa yeye ni mjumbe wa kweli wa Allah Ta’ala’.
“Sauti itaskika angani ikisema, ‘Kwa kweli, mja wangu amezungumza ukweli (na akajibu maswali kwa usahihi), kwa hivyo mtandikie mkeka miongoni ya mikeka ya Jannah, mvishe mavazi ya Jannah, na mfungulia (kaburini mwake) mlango wa Jannah! Harufu ya Jannah itamfikia, na kaburi lake litapanuliwa kwa ajili yake mpaka sehemu macho yake yanaweza kuona.
“Mtu atakuja kwake na uso mzuri, mavazi mazuri na harufu nzuri. Mtu huyo atamwambia, ‘Furahiya juu ya yale ambayo yatakufurahisha! Siku yako hii ndio uliyoahidiwa (kukutana na wakati ulipokuwa ulimwenguni)! ‘Marehemu atamuuliza,’ Wewe ni nani? Uso wako ni uso wa mtu anayeleta wema! ‘Mtu huyo atajibu,’ Mimi ni matendo yako mema. ‘
“Marehemu atasema, ‘Ewe Mola wangu! Anzisha Qiyaamah! Ewe Mola wangu! Anzisha Qiyaamah, ili niweze kurudi na familia yangu na mali zangu (peponi)!'”
Rasulullah (Sallallahu ‘Alaihi Wasallam) kisha akasema, “Kwa kweli, wakati kafiri anakaribia kuondoka duniani na kwenda Akhera, basi malaika hushuka kwake kutoka mbinguni. Malaika hawa wana uso mweusi na watakuwa na magunia ya kitambaa laini. Watakaa karibu naye, sehemu ambao anaweza kuwaona.
“Baada ya hapo, malaika wa kifo atakuja kwake na kukaa kando ya kichwa. Malaika wa kifo atamwambia, ‘Ewe roho mbaya na chafu’! Toka na uje katika ghadhabu ya Allah!. Roho itaanza kuangaika mwilini (ikijaribu kumkimbia malaika wa kifo kuikamata). Baada ya hapo, Malaika wa Kifo atatoa kwa nguvu roho, kama jinsi sindano inavyotolewa kwa nguvu kwenye uzi yakuroana. Malaika wa kifo basi atatoa roho.
“Baada ya malaika wa kifo kushikilia roho, malaika wengine pamoja naye hawataiacha mikononi mwake kwa sikonde moja hadi watakapochukua na kuiweka kwenye gunia. Harufu mbaya itatoka kwenye roho, kama harufu mbaya zaidi maiti inaweza kupatikana duniani.
“Malaika basi watapanda mbinguni na roho, na kikundi chochote cha malaika wanaopita, malaika hao watauliza kutoka kwao, ‘Roho mbaya na chafu hii ni ya nani? Watajibu ni roho ya fulani bin fulani, kumtaja na majina mabay ambayo alikuwa akiitwa duniani.
“Malaika basi wanaendelea kupaa na roho hadi watakapofika mbingu la kwanza. Wakifika mbingu la kwanza, wataomba ruhusa ya kuingia, lakini mlango wa mbinguni hautafunguliwa kwa ajili yao.”
Alipotaja hii, Rasulullah (Sallallahu ‘Alaihi Wasallam) alisoma aya ifuatayo ya Qur’an Majeed:
لَا تُفَتَّحُ لَهُمْ أَبْوَابُ السَّمَاءِ وَلَا يَدْخُلُونَ الْجَنَّةَ حَتَّىٰ يَلِجَ الْجَمَلُ فِي سَمِّ الْخِيَاطِ
Milango ya mbingu haitafunguliwa kwa ajili yao (makafiri), na hawataingia peponi hadi ngamia atakapopita kwenye jicho la sindano (yaani hawataweza kuingia Jannah). (Surah A’raaf aya 40)
Rasulullah (Sallallahu ‘Alaihi Wasallam) kisha akaendelea na akasema, “Mwenyezi Mungu (subhaanahu wata’ala) atasema,’ Andika katika kitabu chake kwamba makao yake yameamuliwa kuwa katika Sijjeen, katika ardhi ya chini kabisa (yaani huko Jahannum). ‘Baadaye, roho yake itatoka kwa nguvu.”
Rasulullah (Sallallahu ‘Alaihi Wasallam) kisha akasoma aya ifuatayo ya Qur’an Majeed:
وَمَن يُشْرِكْ بِاللَّهِ فَكَأَنَّمَا خَرَّ مِنَ السَّمَاءِ فَتَخْطَفُهُ الطَّيْرُ أَوْ تَهْوِي بِهِ الرِّيحُ فِي مَكَانٍ سَحِيقٍ
Yoyote anayemshirikisha Mwenyezi Mungu (subhaanahu wata’ala) , ni kama anaanguka chini kutoka angani, na ndege humnyakua, au upepo humtupa mbali. (Surah Haj aya. 31)
Rasulullah (Sallallahu alaihi wasallam) akaendelea na kusema, “Nafsi yake inarudishwa kwenye mwili wake, na watamjia Malaika wawili (Munkar na Nakeer) wakimkalisha na kumuuliza: ‘Mola wako ni nani?’ Atajibu, ‘Aah! Aah! Mimi sijui!’ Kisha watamuuliza, ‘Dini yako ni ipi?’ Atasema, ‘Aah! Aah! Sijui!’ Hatimaye, malaika watamwuliza, ‘Huyu ni nani aliyetumwa kwako?’ Tena, atajibu, ‘Aah! Aah! sijui!’
“Hapo sauti itaita kutoka mbinguni ikisema: ‘Amesema uwongo, basi mtandilie zulia la moto, na umfungulie mlango wa Moto wa Jahannamu.’ Hivyo, joto la moto na moto mkali wa Jahannam utamfikia, na kaburi lake litabanwa na kupungukiwa juu yake, mpaka (atabanwa kiasi kwamba) mbavu zake kutoka upande mmoja zitaungana na mbavu za upande mwingine.
“Kisha atakuja mtu ambaye sura yake itakuwa ya kutisha, ambaye mavazi yake yatakuwa machafu na ambaye harufu yake itakuwa mbaya zaidi, mtu huyo atamwambia, ‘Furahia kwa kile ambacho kitakuhuzunisha! Siku yako hii ndiyo uliyoahidiwa (tangu ukiwa duniani)!’ Marehemu atamuuliza mtu huyo, ‘Wewe ni nani, kwani uso wako ni uso wa yule anayeleta maovu?’ Atajibu, ‘Mimi ni matendo yako mabaya.
“Maiti atasema: ‘Ewe Mola wangu! Usije Qiyaamah!
Katika riwaya nyingine, imetajwa kwamba nafsi ya Muumini mchamungu inapopanda kuelekea mbinguni, basi kila Malaika baina ya mbingu na ardhi, na kila malaika katika kila mbingu, humswalia. Milango ya mbingu inafunguliwa kwa ajili yake, na Malaika katika kila mlango wanamuomba Allah Ta’ala kwamba nafsi hii takatifu ipae kupitia mlango wao.
Nafsi ya kafiri inapotolewa hutoka na mishipa (yaani itatoka katika kila mshipa wa mwili wake). Kila malaika baina ya mbingu na ardhi, na kila malaika katika kila mbingu, anamlaani. Milango ya mbingu imefungwa, na Malaika katika kila mlango wanamwomba Allah Ta’ala kwamba roho yake isipae kupitia mlango wao.
يَوْمَ تَرْجُفُ الرَّاجِفَةُ ﴿٦﴾ تَتْبَعُهَا الرَّادِفَةُ ﴿٧﴾ قُلُوبٌ يَوْمَئِذٍ وَاجِفَةٌ ﴿٨﴾ أَبْصَارُهَا خَاشِعَةٌ ﴿٩﴾ يَقُولُونَ أَإِنَّا لَمَرْدُودُونَ فِي الْحَافِرَةِ ﴿١٠﴾ أَإِذَا كُنَّا عِظَامًا نَّخِرَةً ﴿١١﴾ قَالُوا تِلْكَ إِذًا كَرَّةٌ خَاسِرَةٌ ﴿١٢﴾ فَإِنَّمَا هِيَ زَجْرَةٌ وَاحِدَةٌ ﴿١٣﴾ فَإِذَا هُم بِالسَّاهِرَةِ ﴿١٤﴾
(Mtafufuliwa) siku ambayo tukio la kutikisika litasababisha kila kitu kutikisika kwa nguvu, (pamoja na) tukio lingine la kutikisika litakalofuata (yaani talumbeta litapulizwa kwa mara ya kwanza, na kupulizwa kwa mara ya pili baada ya muda wa miaka arobaini). Nyoyo (za watu), siku hiyo zitakuwa na khofu, (na) macho yao yatainama (kwa kuona haya). Watasema (makafiri): “Je! kweli tutarudishwa katika hali yetu ya kwanza (baada ya kufufuliwa)? Hata baada ya kuwa mifupa iliyooza?” Wanasema: “Hata hivyo, itakuwa ni marejeo yenye hasara.” Kisha (talumbeta kupulizwa kwa mara ya pili) itakuwa ni sauti moja tu ya ukali, na ghafla wataamshwa (na kuletwa kuhukumiwa kwenye uwanja wa Hashr).
Alislaam Juhudi za Kuleta uislam ndani ya maisha yetu