Hakuna nafasi katika Uislamu kwa wale wanaowatukana Maswahabah (Radhiya Allaahu ‘anhum)

Wakati mmoja, mtu mmoja alikuja kwa Zainul ‘Aabideen, ‘Ali bin Husein (rahimahullah), na kumuuliza:

“Ewe mjukuu wa Mtume (Sallallahu ‘alaihi wasallam)! Nini maoni yako kuhusu ‘Uthmaan (Radhiya Allaahu ‘anhu)?” Kuona chuki ya mtu huyo kwa ‘Uthmaan (Radhiya Allaahu ‘anhu), Zainul ‘Aabideen (Rahimahullah) akamueleza kwamba kwa ujumla, kuna makundi matatu ya Waislamu ambayo yametajwa katika Qur-aan Takatifu (Muhaajirin, Answaar na waliokuja baadae na wakawafuata Muhajirina na Answaar katika matendo mema). Yeye basi akamuuliza, “Ndugu yangu, je wewe ni katika kundi la kwanza la watu (Muhaajireen), ambao Allah Ta’ala anawazungumzia katika Aya ifuatayo ya Qur-aan Takatifu:

 لِلْفُقَرَآءِ ٱلْمُهَٰجِرِينَ ٱلَّذِينَ أُخْرِجُوا۟ مِن دِيَٰرِهِمْ وَأَمْوَٰلِهِمْ يَبْتَغُونَ فَضْلًا مِّنَ ٱللَّهِ وَرِضْوَٰنًا وَيَنصُرُونَ ٱللَّهَ وَرَسُولَهُۥٓ أُو۟لَٰٓئِكَ هُمُ ٱلصَّٰدِقُونَ ‎﴿٨﴾

(Kuna sehemu ya mali) kwa Muhajirina mafukara waliotolewa majumbani mwao na ardhi zao, (waliohijiria Madinah kwa ajili ya) kutafuta fadhila kutoka kwa Allah Ta’ala na radhi (zake) na kusaidia (Dini ya) Allah Ta’ala na Mtume wake. Hao ndio wakweli.”

Mtu huyo akajibu, “Hapana! Mimi si katika Muhajirina!” Zainul ‘Aabideen (rahimahullah) basi akasema: “Ikiwa wewe haupo katika kundi la kwanza lililotajwa katika Aayah, basi je wewe ni katika kundi la pili (Answaar) ambalo Allah Ta’ala anawazungumzia katika Aya ifuatayo:

وَٱلَّذِينَ تَبَوَّءُو ٱلدَّارَ وَٱلْإِيمَٰنَ مِن قَبْلِهِمْ يُحِبُّونَ مَنْ هَاجَرَ إِلَيْهِمْ وَلَا يَجِدُونَ فِى صُدُورِهِمْ حَاجَةً مِّمَّآ أُوتُوا۟ وَيُؤْثِرُونَ عَلَىٰٓ أَنفُسِهِمْ وَلَوْ كَانَ بِهِمْ خَصَاصَةٌ وَمَن يُوقَ شُحَّ نَفْسِهِۦ فَأُو۟لَٰٓئِكَ هُمُ ٱلْمُفْلِحُونَ ‎﴿٩﴾

na (pia kuna sehemu ya mali kwa ajili ya) waliokaa Madina na wakaleta Imaan mbele yao (Muhaajirin waliohijiria Madinah) Wanawapenda walio wahijiria (Muhaajirin), na wala hawaoni wivu nyoyoni mwao kwa mali waliyopewa Muhajirina. Wanawapa (Muhajirina) upendeleo kuliko nafsi zao, ijapokuwa umasikini ni sehemu yao. Na yoyote yule aliyekingwa na ubakhili wa nafsi yake hao ndio wenye kufaulu.”

Yule mtu akajibu, “Hapana! Mimi si miongoni mwa Answaar!” Zainul ‘Aabideen (Rahimahullah)
kisha akasema: “Wallahi! kama haupo katika kundi la tatu ambalo Allah Ta’ala Analizungumzia katika Aayah ifuatayo, basi kwa hakika utakuwa nje ya Uislamu (kwani hautokuwa miongoni mwa makundi matatu ya Waislamu). Kundi la tatu ni wale ambao Allah Ta’ala amesema kuwahusu:

‏ وَٱلَّذِينَ جَآءُو مِنۢ بَعْدِهِمْ يَقُولُونَ رَبَّنَا ٱغْفِرْ لَنَا وَلِإِخْوَٰنِنَا ٱلَّذِينَ سَبَقُونَا بِٱلْإِيمَٰنِ وَلَا تَجْعَلْ فِى قُلُوبِنَا غِلًّا لِّلَّذِينَ ءَامَنُوا۟ رَبَّنَآ إِنَّكَ رَءُوفٌ رَّحِيمٌ ‎﴿١٠﴾

na waliokuja baada yao (Muhaajirin na Answaar) wanasema (huku wakiwaombea du’aa Muhaajirin na Answaar), “Mola wetu! Utughufirie sisi na ndugu zetu waliotutangulia na Imaan, wala usiache katika nyoyo zetu uovu wowote kwa Waumini. Mola wetu! Hakika wewe ni Mkarimu, Mwenye kurehemu.”

Kwa maneno mengine, Zainul Aabideen (Rahimahullah) alimueleza mtu huyo kwamba ikiwa yeye hayupo kwenye kundi la Muhaajirin na Answaar, basi ili awe Muislamu, itamlazimu kuwapenda Muhaajirin na Answaar na kuwafuata katika Dini. (Tafseer Qurtubi 18/31).

About admin

Check Also

Mshale Wa Kwanza Kurushwa kwa Ajili Ya Uislamu

Sa’d (radhiya allaahu ‘anhu) alikuwa miongoni la kundi la Maswahabah ambao Mtume (sallallahu ‘alaihi wasallam) …